UTANGULIZI
Leo ni takriban mwaka mmoja na robo tatu tangu John Pombe Magufuli ale kiapo cha kuwa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mengi yametokea katika kipindi hiki cha karibu miaka miwili. Rais Magufuli amepiga marufuku shughuli za kisiasa, hasa mikutano ya hadhara na maandamano yanayoruhusiwa na Katiba pamoja na Sheria ya Vyama vya Siasa.
Amesitisha ama kushambulia vikali haki na uhuru wa kikatiba wa wananchi kupashana habari na/au kutoa maoni yao juu ya masuala mbali mbali yanayohusu nchi yao. Amebomoa uhuru wa vyombo vya habari kwa kutishia uhai wao na kwa kushambulia wanahabari na/au kuwakamata na kuwashtaki.
Amevuruga taratibu za utumishi wa umma kwa ‘kutumbua’ watumishi wa umma wa kada mbali mbali na kuweka wapambe wake wa kisiasa na/au ndugu, jamaa na hata marafiki zake katika nafasi nyeti za utumishi wa umma. Amevuruga uhuru wa Bunge na Mahakama kama vyombo vya udhibiti na uwajibikaji wa serikali.
Kwa kipimo chochote kile, Tanzania ya Magufuli imegeuka kuwa dola la kidikteta na kikandamizaji, linalotegemea zaidi mabavu ya vyombo vya ulinzi na usalama.
HAKUNA ALIYEBAKI SALAMA!!!
Kama tulivyosema mwezi Julai ya mwaka jana wakati tunatangaza kunzishwa kwa Umoja wa Kupinga Udikteta Tanzania (UKUTA), nchi inapoingia katika utawala wa kidikteta, hakuna mtu anayeweza kubaki salama. Ndivyo ambavyo imetokea katika Tanzania ya Magufuli. Hakuna kundi la kijamii ambalo limebaki salama. Wafanyakazi wa sekta za umma na binafsi wameathirika, kama ambavyo imetokea kwa wanafunzi wa ngazi mbali mbali za elimu.
Wafanyabiashara, kwa muda mrefu marafiki na wachangiaji wakubwa wa CCM, nao ‘wameisoma namba’ ya Magufuli kwa namna ambayo leo hii ni vigumu kufanya biashara yoyote kwa sababu ya kodi za kinyang’anyi na kibano cha TRA. Wenye magari nao wameisoma namba kwa sababu ya utitiri wa tochi za barabarani na faini za ajabu ajabu zinazotozwa na askari polisi wa usalama barabarani. Wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiri amali wa kila aina nao wameathiriwa na miaka hii miwili ya utawala wa Rais Magufuli.
Lakini katika matendo yote ya utawala wa Rais Magufuli, hakuna ambalo limeishangaza nchi yetu na dunia kwa ujumla kama vita aliyoianzisha dhidi ya wawekezaji na wafanyabiashara wengine wa kigeni katika sekta mbali mbali za uchumi wa nchi yetu.
Sio tu kwamba Rais Magufuli amekamata na kuzuia usafirishaji nchi za nje wa ‘mchanga wa dhahabu’ wa kampuni ya uchimbaji ya Acacia Mining PLC; sio tu kwamba ameshinikiza kampuni hiyo kupigwa faini ya dola za Marekani bilioni 194 – ambayo haijawahi kutokea mahali pengine popote duniani – kwa kutumia hoja za kupikwa za wasomi uchwara.
Bali pia Rais Magufuli, kwa kutumia Bunge – ambalo sasa linatumika kama muhuri wa kubariki kila jambo analotaka yeye na Serikali yake – ametunga Sheria zinazohusu udhibiti wa maliasili, ambazo zimevunja, kukiuka au kubadilisha kila mkataba au makubaliano ambayo Tanzania imewahi kufanya na mwekezaji yeyote wa nje kuhusu matumizi na udhibiti wa maliasili katika kipindi chote cha miaka ya nyuma.
Mabadiliko haya ya kisheria yamefanyika bila kuzingatia haki na wajibu wa Serikali ya Tanzania na wawekezaji hao kwa mujibu wa sheria za kimataifa, mikataba ya kimataifa, sheria zetu wenyewe na mikataba iliyoingiwa kati ya Serikali na wawekezaji wa nje. Kisheria mabadiliko haya yanachukuliwa kama ‘unyanganyi wa nguvu’ (compulsory acquisition) au ‘utaifishaji’ (nationalization) ambao umepigwa marufuku na Katiba ya nchi yetu kama hauna “idhini ya sheria ambayo imeweka masharti ya kutoa fidia inayostahili.”
TUSIOGOPE KUSHTAKIWA???
Matokeo ya matendo haya ya Serikali ya Rais Magufuli ni kwamba sasa nchi yetu imeingia katika mgogoro mkubwa na wawekezaji wa nje katika sekta mbali mbali za uchumi wa nchi yetu. Tangu sheria mpya zipitishwe na kuidhinishwa na Magufuli, makampuni makubwa ya uchimbaji madini duniani yenye vitega uchumi Tanzania yameanzisha utaratibu wa kufungua mashtaka dhidi yetu katika mahakama za kimataifa za usuluhishi wa migogoro ya uwekezaji.
Acacia Mining PLC, inayomiliki mchanga wa dhahabu uliokamatwa kwa amri ya Magufuli na yenye Migodi ya Dhahabu ya Bulyanhulu, Buzwagi na North Mara Tarime, tayari imekwishatoa taarifa rasmi ya kutufungulia mashtaka. AngloGOld Ashanti, inayomiliki Mgodi wa Dhahabu wa Geita ambao ndio mgodi mkubwa kuliko yote Tanzania, nayo imekwishatoa taarifa rasmi ya kutushtaki.
Na kwa taarifa tulizo nazo, makampuni mengine ya uwekezaji katika sekta za uchimbaji madini, gesi asilia na mafuta nayo yameanzisha mchakato wa kufungua mashtaka katika mahakama za kimataifa dhidi ya Tanzania. Kwa kifupi, kwa sababu ya matendo ya Rais Magufuli yasiyozingatia mazingira halisi ya kiuchumi na kisheria kati yetu na nchi au taasisi za kiuchumi za kimataifa, Tanzania itajikuta ikishtakiwa na kudaiwa mabilioni ya fedha za kigeni katika mahakama za kimataifa.
Hata hivyo, mjadala wa masuala haya ulipoibuka Bungeni wakati wa Bunge la Bajeti la mwaka huu, mawaziri – ambao ndio washauri wa Rais kwa kujibu wa Katiba yetu – walitamka hadharani kwamba Tanzania ni nchi huru kwa hiyo haitakiwi kuogopa kushtakiwa katika mahakama za nje. Mawaziri hawa, baadhi yao wakiwa wasomi wakubwa wa sheria hapa nchini, wamempotosha Rais Magufuli na kuliweka taifa letu katika hatari kubwa.
BOMBARDIER NYINGINE IKO WAPI???
Mwaka jana Rais Magufuli alipokea ndege mbili za aina ya Bombardier Q400 zilizotengezwa Canada kwa mbwembwe na shamra shamra kubwa. Licha ya ununuzi wa ndege hizo kuacha maswali mengi bila kujibiwa, Rais Magufuli aliahidi kwamba Serikali yake ilikuwa imeagiza Bombardier nyingine mbili na Boeing 787 ‘Dreamliner’ moja kampuni ya Boeing ya Marekani. Tuliambiwa kwamba mojawapo ya Bombardier hizo ingewasili Tanzania mwezi Julai ya mwaka huu, wakati Bombardier ya pili na Dreamliner zingewasili nchini mwakani.
Hadi sasa Bombardier iliyotarajiwa kuwasili mwezi uliopita haijaonekana bado. Na Serikali ya Rais Magufuli imepatwa na kimya cha ghafla. Siku mbili zilizopita, baada ya Mbunge Zitto Kabwe kuuliza Bombardier iliyoahidiwa kufikia mwezi Julai iko wapi, Waziri wa Uchukuzi Profesa Makame Mnyaa Mbarawa alijibu haraka haraka kwamba bado kuna mambo yamakamilishwa na ndege yetu itakuja muda si mrefu. Profesa Mbarawa hajasema ukweli. Bombardier ya Magufuli imekamatwa na inashikiliwa Canada na wadeni wetu.
NINI KIMETOKEA???
Wiki mbili zilizopita Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Dkt. Augustine P. Mahiga alifanya ziara ya kimya kimya nchini Canada. Akiwa huko, Dkt. Mahiga pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Canada, Jack Mugendi Zoka, walifanya mazungumzo na kampuni ya ujenzi ya Stirling Civil Engineering Ltd. ya Montreal, Canada. Mazungumzo hayo yalihusu deni la dola za Marekani 38,711,479 (takriban TAS bilioni 87) inazodaiwa Serikali ya Tanzania kutokana na hukumu mbili za Mahakama ya Usuluhishi zilizotolewa dhidi yetu mwaka 2009 na 2010. Mazungumzo hayo yalihusu pia amri ya kukamatwa kwa mali zote za Tanzania zilizopo mikononi mwa kampuni ya kutengeneza ndege ya Bombardier, “pamoja na ndege ya abiria ya (Bombardier) Q400 iliyokuwa inatazamiwa kukabidhiwa kwa Tanzania mwishoni mwa Julai 2017.”
Miaka ya nyuma wakati Rais John Magufuli akiwa Waziri wa Ujengi, kampuni Stirling Civil Engineering Ltd. iliwahi kupewa kandarasi ya Mradi wa Barabara wa Wazo Hill – Bagamoyo. Kabla ya kukamilisha kandarasi hiyo, na katika mazingira ya ‘ki-Magufuli’, yaani kuvunja mikataba kwa kukurupuka na bila kuzingatia sheria, kampuni hiyo ilinyang’anywa kandarasi hiyo na kutimuliwa nchini. Stirling Civil Engineering Ltd. ikafungua mashtaka katika mahakama ya kimataifa ya usuluhishi.
Mnamo tarehe 10 Desemba, 2009, na baadae tarehe 10 Juni, 2010, mahakama ya usuluhishi ilitoa tuzo ya takriban dola za Marekani milioni 25 pamoja na riba ya 8% hadi malipo kamili yatakapofanyika. Tuzo hiyo imesajiliwa na kutambuliwa kama deni halali la Serikali ya Tanzania kwa Stirling Civil Engineering Ltd. katika nchi za Ufaransa, Uholanzi, Ubelgiji, Uingereza na Uganda.
Licha ya jitihada mbali mbali za kulipwa deni lake, hadi sasa Serikali ya Tanzania haijalipa deni hilo ambalo sasa, kwa sababu ya ucheleweshaji wa malipo, limeongezeka hadi dola za Marekani 38,711,479 kufikia tarehe 30 Juni, 2017. Hapo ndipo Stirling Civil Engineering Ltd. ilipoamua kuomba amri ya Mahakama Kuu ya Montreal ya kukamata mali zote za Tanzania zilizopo kwa kampuni ya Bombardier, zikijumuisha ndege ya Bombardier Q400.
Katika mazungumzo yake na kampuni ya Stirling Civil Engineering Ltd., Waziri Mahiga ‘alisisitiza umuhimu wa kuepuka suala hili kujulikana hadharani.’ Kwa upande wake, kampuni ya Stirling Civil Engineering Ltd. imekubali kuiachia ndege ya Bombardier Q400 kwa malipo ya mwanzo ya dola za Marekani milioni 12.5 na baadae itatuma ujumbe wake Tanzania kwa ajili ya kuja kufanya makubaliano ya mwisho juu ya kulipa deni hilo. Endapo malipo hayo yatafanywa na Serikali, Stirling Civil Engineering Ltd. ‘itaondoa tishio la mnada wa lazima wa Bombardier Q400 na kujulikana hadharani’ kwa mgogoro huo.
KWA NINI KUKAMATWA KWA BOMBARDIER NI MUHIMU???
Suala la kukamatwa kwa ‘Bombardier ya Magufuli’ linaibua maswali mengi yanayohitaji majibu ya Rais Magufuli na Serikali yake. Kwanza, ni kwa sababu gani Waziri (wakati huo) Magufuli alivunja mkataba wa Stirling Civil Engineering Ltd., kitendo ambacho kimepelekea Serikali kuingia hasara ya mabilioni ya shilingi???
Pili, kwa nini deni la Stirling Civil Engineering Ltd. halikulipwa mara baada ya mahakama ya usuluhishi kutoa tuzo ya dola za Marekani milioni 25, kitendo ambacho kimesababisha deni hilo sasa kufikia dola milioni 38.711??? Tatu, msisitizo wa Waziri Mahiga kwamba suala hili lifanywe kwa siri na lisitangazwe hadharani ulikuwa unalenga kumlinda nani na kwa nini???
Haya ni maswali muhimu kupatiwa majibu ya kweli na sahihi. Kusababisha hasara kwa mamlaka ya serikali ni kosa kubwa la jinai la ufisadi kwa mujibu wa Sheria ya Uhujumu Uchumi. Mawaziri wa zamani Daniel Yona na Basil Mramba, waliopatikana na hatia ya kusababisha hasara ya shilingi bilioni 9 kwa Serikali kwa kitendo chao cha kutoa msamaha wa kodi kwa kampuni ya Alex Stewart Assayers ya Marekani, walihukumiwa kifungo jela kwa kosa hili.
Na tangu aingie madarakani, Rais Magufuli mwenyewe ‘ametumbua’ maofisa wengi wa Serikali na taasisi mbali mbali za umma kwa kusababisha hasara kwa Serikali. Wengi wa maofisa hao wamefunguliwa mashtaka ya jinai ya uhujumu uchumi au utakatishaji haramu wa fedha. Wengi wao wanaendelea kusota mahabusu kwa sababu makosa haya hayana dhamana.
Sasa tunataka kujua nani atakayewajibika kijinai kwa kulisababishia taifa letu hasara ya shilingi bilioni 87 ambayo imepelekea Bombardier yetu na mali zetu nyingine kukamatwa nchini Canada.
Kwenye suala hili, Rais Magufuli hawezi kujificha kwenye kichaka cha Katiba cha kinga ya Rais dhidi ya mashtaka ya jinai. Kwa mujibu wa ibara ya 46(3) ya Katiba yetu, kinga hiyo ipo kwa ajili ya “… jambo lolote alilolifanya yeye kama Rais wakati alipokuwa bado anashika madaraka ya Rais kwa mujibu wa Katiba hii.”
Magufulu hakuwa Rais mwaka 2009 wakati anavunja mkataba wa Stirling Civil Engineering Ltd., na mwaka 2010 wakati tunabambikwa kulipa tuzo ya dola milioni 25. Na wala hakuwa Rais mwaka 2014 wakati Serikali ya Tanzania inashindwa kutekeleza mapatano ya kumaliza mgogoro huu ambapo Serikali iliwekewa masharti nafuu ya kulipa deni pamoja na kupata punguzo kubwa la deni hilo.
SIO MARA YA KWANZA!!!
Kwa bahati mbaya, hii sio mara ya kwanza kwa Rais Magufuli kuiingiza nchi yetu kwenye hasara kubwa kwa sababu ya kufanya kwa kukurupuka na bila kuzingatia sheria za nchi. Mwezi Septemba mwaka jana, kampuni ya Sea Tawariq LLC ya Muscat, Oman, ilifungua madai ya zaidi ya shilingi bilioni 6 kama fidia ya meli na samaki waliokamatwa na Serikali ya Tanzania katika kesi maarufu ya ‘Samaki wa Magufuli.’
Meli hiyo na mzigo wake wa samaki ilikamatwa mwaka 2008 kwa amri ya Magufuli, wakati huo akiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi. Aidha, akiwa Waziri wa Ujenzi, Magufuli aliwahi kuamuru kubomolewa kwa kituo cha mafuta jijini Mwanza, kitendo kilichopelekea Serikali kushtakiwa mahakamani na kuamriwa kulipa fidia ya mabilioni ya fedha kwa mmiliki wa kituo hicho.
Na wala hii sio mara ya kwanza kwa nchi yetu kubebeshwa mzigo mkubwa wa madeni yanayotokana na maamuzi ya kukurupuka ya mawaziri na viongozi wetu wengine wa ngazi za juu. Symbion Power (Tanzania) Ltd., warithi wa kampuni ya kuzalisha umeme ya Dowans inaidai Serikali mabilioni mengi ya shilingi kutokana na kutolipwa kwa umeme inayozalisha Ubungo chini ya Mkataba wa Kununua Umeme na Leseni ya Kufua Umeme iliyotolewa kwa kampuni hiyo tarehe 10 Desemba, 2015. Licha ya kuzalisha umeme na kuuingiza kwenye gridi ya taifa, kampuni hiyo imekuwa ikiambiwa na Serikali ya Rais Magufuli kwamba mkataba wao ‘unapitiwa upya.’ Kwa mwenendo huu, haitakuwa ajabu kusikia baadae kwamba mali nyingine za nchi yetu zimekamatwa nchi za nje ili kulipa madeni ya aina hii.
NINI KIFANYIKE???
Katika mazingira haya, mambo yafuatayo yanatakiwa kufanyika. Kwanza, Serikali ya Rais Magufuli lazima iwajibishwe. Kwa sababu sasa ni Rais, Magufuli ana kinga dhidi ya mashtaka ya aina yoyote ya jinai kwa mujibu wa ibara ya 46(1) ya Katiba. Hii ni licha ya ukweli kwamba alifanya makosa haya kabla hajawa Rais.
Kwa sababu hiyo, na licha ya mazingira magumu ya kisiasa na kibunge, Bunge la Jamhuri ya Muungano linatakiwa kuchukua jukumu la kuunda Kamati Teule ya Bunge kuchunguza suala hili na masuala mengine ya uvunjaji wa sheria na mikataba ambayo imepelekea nchi yetu kuingia hasara kubwa.
Pili, Bunge, vyama vya siasa vyenye maslahi ya kweli ya nchi yetu pamoja na wananchi kwa ujumla, wanatakiwa kuishinikiza Serikali ya Rais Magufuli kuweka hadharani kesi zote ambazo zimefunguliwa au zinatarajiwa kufunguliwa dhidi ya nchi yetu katika mahakama za kimataifa za usuluhishi ili wananchi wapate kufahamu gharama na hasara ambazo nchi yetu inakabiliwa nazo kwa sababu ya ukosefu wa umakini katika kushughulikia mikataba kati yetu na taasisi za kibishara za kimataifa.
Makosa makubwa yamefanyika na yataendelea kufanyika kwa sababu ya usiri mkubwa unaozunguka maamuzi yanayofanywa na mawaziri na viongozi wetu wa juu wa serikali kuhusu mikataba hiyo. Tayari kuna taarifa kwamba Acacia Mining PLC, AngoGold Ashanti na makampuni mengine ya madini, gesi asilia na mafuta yameshatoa taarifa za kusudio la kutushtaki. Tunataka orodha kamili itolewe hadharani na Rais Magufuli na Serikali yake.
Tatu, ni umuhimu wa kurejesha mjadala wa Katiba Mpya na demokrasia. Mgogoro huu unaonyesha umuhimu na haja ya kuwa na Katiba Mpya na ya kidemokrasia itakayodhibiti mamlaka ya Rais na watendaji wakuu wa Serikali. Katiba ya sasa, kama alivyowahi kusema Mwalimu Nyerere, inampa Rais mamlaka ya kidikteta. Baada ya miaka miwili ya ‘kuisoma namba’ ya Magufuli, na kwa ushahidi wa kukamatwa kwa Bombardier ya Magufuli, ni wazi kwamba tunahitaji Katiba Mpya. Na ni wazi tunahitaji Siasa Mpya. CCM ya Magufuli, kama ilivyokuwa kwa watangulizi wake, ni ile ile.

Share Button