MDAHALO BAINA YA CHADEMA NA CCM

 

Baada ya tamko la Mwenyekiti wa Chama Taifa Mheshimiwa Freeman  Aikaeli Mbowe kuhusu maazimio ya Kamati Kuu ya Chama kuitisha maandamano ya amani tarehe 24 Januari, 2024 Jijini Dar Es salaam, ameibuka  Katibu wa itikadi na Uenezi wa Chama cha Mapinduzi na kutoa kauli potofu dhidi ya Maazimio ya Kamati Kuu.

 

Ikumbukwe kwamba Maandamano hayo ni sehemu ya vuguvugu la kudai haki nchini, ikiwa na madai ya kuitaka Serikali kuondoa miswada mibovu mitatu Bungeni, kuanzisha mchakato wa mabadiliko madogo ya Katiba ya Mwaka 1977 (minimum reforms), kupunguza ugumu wa maisha na kusikiliza na kuheshimu maoni ya wananchi.

 

Tumesikia kauli ya ya Katibu wa Uenezi wa CCM akitoa rai kuwa anaomba ufanyike mdahalo baina ya viongozi wa Chadema na ‘yeye binafsi’!

 

Msimamo wa Chama ni kuwa kama anataka mdahalo sisi kama  Chama tupo tayari na hatujawahi kukimbia midahalo kama wao na Chama chao, Hivyo basi mdahalo unaweza kufanyika katika masuala yafuatayo ambayo tumeweka msimamo wetu wazi ili yatekelezwe na Serikali;

 

  1. Serikali iondoe kwanza miswada mitatu mibovu Bungeni; ili kuwezesha wadau mbalimbali tukae kwenye mdahalo wa kujadili maudhui ya Miswada ya Sheria za Uchaguzi, Tume ya Uchaguzi na Sheria zinazohusu masuala ya Vyama vya Siasa.

 

  1. Serikali ianzishe mara moja mchakato wa marekebisho ya Katiba ya Mwaka 1977 (Minimum reforms) ili kuwezesha kuondoa mapungufu yaliyopo kwenye Katiba hiyo ili kuruhusu maandalizi ya kuandikwa Kwa miswada mipya ya kuboresha mifumo ya chaguzi nchini.

 

  1. ⁠Serikali iwasilishe Bungeni muswada wa Sheria ya kusimamia Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi huo usimamiwe na Tume ya Uchaguzi badala ya TAMISEMI.

 

  1. ⁠Serikali iwasilishe Bungeni muswada wa Sheria wa kukwamua mchakato wa Katiba Mpya ukiwa na mwelekeo (Road Map)wa lini nchi itapata Katiba Mpya.

 

  1. ⁠Wadau tutaweza kukaa kwenye mdahalo ili kuishauri Serikali jinsi ya kuweza kupunguza ukali wa gharama za maisha na kuonyesha Kodi na tozo zipi zipunguzwe,anasa gani ziondolewe Serikalini, na mkakati mzima wa kupunguza ukali wa gharama za maisha kwa wananchi .

 

Aidha, tunamkumbusha Mwenezi wa CCM kuwa Miswada hii imepelekwa Bungeni na Serikali na imepuuza maoni ya wananchi, Viongozi wa dini, Wadau na vyama vya siasa, ripoti za waangalizi wa Uchaguzi wa kimataifa na ndani, Taarifa ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Mwaka 2020 pamoja na amri za Mahakama ya Afrika na Afrika Mashariki kuhusu maeneo mahususi ya kuboresha mifumo ya chaguzi na Sheria ya Vyama.

 

Hivyo basi katika kipindi hiki aweke mdahalo na Serikali ili waone ulazima wa kusikiliza na kuheshimu maoni ya wananchi na wadau mbalimbali wa chaguzi katika kuandaa mazingira Bora ya kuwa na chaguzi huru na haki nchini.

 

Katika kipindi hiki Chama kinaendelea na maandalizi ya maandamano ya amani yatakayofanyika Jijini Dar Es salaam tarehe 24 Januari, 2024.

 

Imetolewa leo Jumatatu  tarehe 15 Januari, 2024

John Mrema

Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya nje.

Share Button